Na John Banda, Dodoma
MSAJILI wa Hazina,Lawrence Mafuru amekiri kuwa bado
kuna msururu wa mashirika ya umma ambayo kila siku yanapanga foleni Hazina
kwaajili ya kusaidiwa huku mengine yakisaidiwa kulipiwa mishahara ingawa yanafanya
biashara.
Kauli hiyo aliitoa jana katika kikao cha Kamati ya
bunge ya hesabu za serikali(PAC) ilipokuwa ikihoji hoja za Mkaguzi Mkuu wa
hesabu za serikali(CAG) kwa benki ya posta Tanzania, mjini hapa.
Mafuru alisema kwasasa inajidhihirisha na kuondoa hisia kuwa
mashirika ya umma yanayomilikiwa na serikali hayawezi kuendeshwa kwa ufanisi.
Alibainisha licha ya hisia hizo lakini bado Hazina
kuna msururu wa mashirika yanayosaidiwa ingawa yanajiendesha kibiashara.
“Lakini hapa tunapata ushahidi tukiyasimamia vizuri
mashirika yetu na kuyasaidia yanaweza kujiendesha na kuleta tija na kupata
faida,”alisema Mafuru
Hata hivyo alisema kwa jitihada zilizofanywa na
benki ya posta inapeleka meseji kwa mashirika mengine kwamba hakuna kisingizio inawezekana
kujiendesha kwa ufanisi na tija.
Alisema maagizo yaliyotolewa na kamati hiyo yatasaidia benki
ya posta kufikia malengo yake.
“Benki iendelee kujiimarisha na kuyafanya mashirika
mengine yatakayoingia kwenye kamati ya PAC kujipanga na kuonesha kwa namna gani
inaweza kuwasaidia watanzania kwa kujiendesha kwa faida kupitia miradi ya
maendeleo, naipongeza Benki hii kwa sasa kujiimarisha tofauti na ilipokuwa
mwanzo,”alisema Msajili huyo
Alibainisha benki hiyo kwasasa ipo kibiashara na ipo
kwenye nafasi ya juu kati ya zaidi ya benki 50 na kwamba taasisi kama hizo
kwasasa zinatakiwa kujiendesha kibiashara na kuyataka mashirika mengine
kujifunza katika hilo.
Mafuru alisema inawezekana kujiendesha na
kutengeneza faida badala ya kuwa tegemezi na hivyo utamaduni huo uigwe na
mashirika mengine.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Aeshi Hilaly,
aliipongeza benki hiyo kwa kufikia mtaji wa sh. Bilioni 41 ambapo alisema
ilikuwa kwenye mtaji wa chini sana hapo awali na kuonekana ikielekea kufa.
Naye Mwenyekiti wa bodi ya benki hiyo, Profesa
Lettice Rutashobya, alisema atashughulikia mapungufu yaliyojitokeza katika
ukaguzi ili mwaka ujao kusiwe na hoja hizo.
Aidha alisema atahakikisha benki hiyo inajiimarisha
na hatarudi katika hali iliyokuwa awali kutokana na mikakati iliyopo ikiwa ni
pamoja na kufunga mifumo mbalimbali ili kuwa na uwezo wa kushindana na benki
zingine.
Mwisho.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni